FECAFOOT yakana ujio wa kocha mpya

Shirikisho la Soka nchini Cameroon ‘FECAFOOT’ limekanusha na kushangazwa na Wizara ya Michezo ya nchi hiyo kumteua Marc Brys kuwa Kocha Mkuu mpya wa timu ya taifa, ‘Indomitable Lions’.

Kocha huyo raia wa Ubelgji mwenye umri wa miaka 61, amechaguliwa kuchukua nafasi ya mlinzi wa zamani wa Liverpool na West Ham, Rigobert Song.

Hata hivyo, FECAFOOT katika taarifa yake imesema haikuwa na taarifa yoyote kwani haikuhusishwa kuhusu ajira ya kocha huyo. Baraza la Michezo la nchi hiyo limesema litafuatilia suala hilo la kusikitisha kujua ukweli kamili.

Mshambuliaji wa zamani wa FC Barcelona, Inter Milan na Chelsea, Samuel Eto’o ndiye Rais wa FECAFOOT tangu Desemba, 2021. Kwa sasa anachunguzwa na Shirikisho la Soka Barani Afrika ‘Caf’ kwa madai ya utovu wa nidhamu.

Wizara ya Michezo imesema Brys atasaidiana na Joachim Mununga na Giannis Xilouris, lakini ingawa haikusema mkataba wa kocha huyo ni wa muda gani.

Mshambuliaji wa zamani wa Cameroon, Francois Omam-Biyik aliyeshiriki fainali tatu za Kombe la Dunia, ni miongoni mwa watu walioongezwa katika benchi la ufundi la timu hiyo. Wateuliwa wengine ni upande wa tiba na utawala.

Song, mchezaji wa zamani wa kimataifa wa Cameroon aliteuliwa kuiongoza timu hiyo mwaka 2022 kwa amri ya Rais wa nchi hiyo, Paul Biya, lakini mkataba wake ulikamilika mwishoni mwa Februari.

Aliongoza Indomitable Lions kwenye Kombe la Dunia la 2022 nchini Qatar ambako waliwafunga mabingwa mara tano Brazil, lakini waliishia hatua ya makundi.

Hivi karibuni Cameroon ilitolewa katika hatua ya 16 bora ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika ‘AFCON 2023’ na Nigeria ambao walicheza Fainali na kufungwa mabao 2-1 na wenyeji Ivory Coast waliotwaa ubingwa.

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii