Wezi waliiba mali yenye thamani ya makumi ya mamilioni ya euro kutoka kwenye masanduku ya kuhifadhia fedha na vito vya thamani ndani ya benki moja nchini Ujerumani.
Polisi imesema wezi hao walifanya wizi huo Jumatatu kwa kutumia ukimya uliokuwepo wakati wa mapumziko ya siku kuu.
Wapelelezi wanakadiria kwamba waliiba takriban euro milioni 30 wakati wa uvamizi wa benki ya Sparkasse katika jiji la Gelsenkirchen lililoko magharibi mwa nchi. Msemaji wa polisi alielezea uvamizi huo kuwa wa utaalamu wa hali ya juu, akisema ulihitaji mipango mikubwa, ushirikiano na mtu anayefanya kazi ndani ya benki hiyo, na azma kubwa ya kuutekeleza uhalifu huo.
Wavamizi hao walipata njia ya kuingia benki kutoka kwenye gereji ya kuegesha magari, wakitoboa shimo kubwa ndani ya chumba cha kuhifadhia vitu na baadaye wakatoroka kupitia njia hiyo hiyo wakiwa na vitu vilivyoibwa.
Zaidi ya masanduku 3,000 ya kuhifadhia vitu katika chumba maalum yalifunguliwa kwa nguvu, yakiwa na pesa taslimu, vito vya thamani, na dhahabu.
Wizi huo ulibainika Jumatatu baada ya king'ora kusikika na kuwaarifu wahudumu wa dharura.
Mashahidi waliwaambia polisi kwamba waliona wanaume kadhaa wakiwa wamebeba mifuko mikubwa kwenye ngazi za gereji ya kuegesha magari usiku wa Jumapili.