Marekani yasema imerejesha $500m kwa Venezuela

Marekani imerejesha fedha za mauzo ya mwanzo ya mafuta ya Venezuela, ikiwa ni sehemu ya makubaliano baina ya Caracas na Washington yaliyofikiwa mwezi uliopita, baada ya kupinduliwa na kutekwa Rais Nicolas Maduro.

Kwa mujibu wa afisa mmoja wa Marekani anayehusika na makubaliano hayo, sasa nchi yake imekamilisha marejesho ya dola milioni 500, ambazo zitatumika kwa maslahi ya raia wa nchi hiyo chini ya uangalizi wa Washington.

Fedha hizo zimelipwa kwa awamu mbili, kwanza dola milioni 300 na kisha dola milioni 200 zilizokamilishwa siku ya Jumanne (Februari 3).

Wiki iliyopita, Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Marekani, Marco Rubio, aliliambia bunge la nchi yake kwamba fedha hizo ambazo zilihifadhiwa nchini Qatar ni hatua ya dharura kwa ajili ya malipo ya mishahara ya maafisa wa serikali ya Venezuela, wakiwemo wanajeshi, wazimamoto na walimu.

Hata hivyo, mipango ya muda mrefu inatajwa ni kuzishikilia fedha za mauzo ya mafuta nchini Marekani na kutumiwa kwa mujibu wa maelekezo ya Washington. 

#10YrsJembefm  #Familiamoja #AhsantekwaTime

Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii