Mkosoaji wa serikali Kenya Vincent Kipsang atekwa nyara

KUTEKWA nyara kwa mkosoaji mkubwa wa serikali Vincent Kipsang, ambaye alijitangaza Mwenyekiti wa DCP Kaunti ya Baringo kumezua taharuki mjini Kabarnet.

Mfanyabiashara huyo ambaye pia ni bloga anayefahamika kama ‘Zonko Classic’ kwa mujibu wa wenyeji, alidaiwa kutekwa nyara Jumapili jioni na watu wasiojulikana.

Alibebewa juu juu na kuwekwa kwenye subaru kisha wakaondoka naye na hadi leo bado hajulikani aliko.

Bw Kipsang ni mkosoaji mkubwa wa Rais William Ruto na ni kati ya wale ambao wamekuwa wakiendeleza kauli mbiu ya ‘muhula moja’.

Kauli hiyo imekuwa ikishabikiwa Baringo na maeneo jirani.

Kwa mujibu wa mashahidi, alitekwa nyara na watu waliokuwa kwenye Subaru mbili na gari aina ya Toyota Land Cruiser.

Walimchukua kutoka kwa duka lake kisha wakaenda naye eneo kusikojulikana.

Wanafamilia wake, wanaharakati na baadhi ya wanajamii sasa wanadai alitekwa nyara kutokana na sababu za kisiasa kwa sababu ya kukosoa utawala wa Kenya Kwanza mara kwa mara.


Pata Habari Kupitia Mitandao Yetu Ya Kijamii