Kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Tundu Lissu inatarajiwa kuanza kusikilizwa kwa mfululizo kuanzia leo Oktoba 6 hadi Oktoba 24 mwaka huu na kisha kuendelea tena Novemba 3 hadi Novemba 12, mwaka huu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Oktoba 5 mwaka huu na Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uenezi wa CHADEMA, Brenda Rupia, maandalizi yote muhimu kwa ajili ya usikilizwaji wa kesi hiyo yamekamilika rasmi. Taarifa hiyo imeeleza kuwa Lissu yuko imara, thabiti na tayari kushiriki kikamilifu katika hatua zote za usikilizwaji.
“Kwa mujibu wa utaratibu wa mahakama, upande wa Jamhuri utaanza kutoa ushahidi wake. Inatarajiwa kuwa mashahidi wa Jamhuri watakuwa thelathini (30), na vielelezo vitakavyowasilishwa mahakamani ni kumi na moja (11),” imeeleza taarifa hiyo.
CHADEMA imewataka Watanzania wote kuendelea kufuatilia mwenendo wa kesi hiyo kwa umakini, na kusimama pamoja na Mwenyekiti wao katika kudai haki, ukweli, na misingi ya demokrasia pamoja na utawala wa sheria.