Waziri wa Nigeria wa Ubunifu Sayansi na Teknolojia Uche Nnaji amejiondoa madarakani siku chache baada ya kuibuka kwa madai ya kwambakulikuwa na udanganyifu katika cheti chake cha elimu.
Katika uchunguzi uliofanywa kwa muda wa miaka miwili ulionyesha kuwa Nnaji alidai kuwasilisha vyeti vya kughoshi kwa Rais Bola Tinubu wakati wa uteuzi wake wa kuwa waziri mwaka 2023.
Aidha msemaji wa Rais Bayo Onanuga alithibitisha kujiuzulu kwa Nnaji kupitia chapisho lake kwenye mtandao wa X akimuunga mkono Nnaji kuwa hizi ni “vita za kisiasa kutoka kwa yam pinzani”.
Nnaji amekana madai ya udanganyifu na ameendelea kudai kuwa alihitimu kutoka Chuo Kikuu cha Nigeria, Nsukka (UNN) akiwa na shahada ya Microbiology/Biochemistry. Hata hivyo UNN iliripoti kwamba haina rekodi zinazoithibitisha kuwa waziri alihitimu shahada ya Bachelor of Science mwaka 1985 kama alivyodai.
Afisa mmoja wa chuo alisema Nnaji alikubaliwa mwaka 1981 lakini hakukamilisha masomo yake wala kupata cheti.
Aidha, National Youth Service Corps (NYSC) ilisema kuwa cheti cha utumishi wa kitaifa alichokuwa amekileta Aprili 2023 hakiwezi kuthibitishwa.
Kiongozi wa upinzani, Atiku Abubakar, ameitaka serikali kufanya uchunguzi huru na wazi kuhusu suala hili, akisema Nnaji anastahili kuachishwa madarakani mara moja na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kwa udanganyifu. “Wanigeria wanastahili kujua ukweli kuhusu wale wanaosimamia maisha na rasilimali zao,” Abubakar aliandika kwenye X.
Kujiuzulu au kusimamishwa kwa waziri ni jambo lisilo la kawaida nchini Nigeria. Nnaji ni waziri wa pili tu kuondoka madarakani tangu Rais Tinubu achukue madaraka mwezi Mei 2023.
Januari iliyopita, Waziri wa Masuala ya Kibinadamu na Kupunguza Umaskini, Betta Edu, alisimamishwa kutokana na kashfa ya ufisadi, ingawa alikanusha makosa yote.