Mwanadiplomasia mkuu wa Iran Abbas Araghchi ameonya kwamba jaribio lolote la meli kupuuza njia mbadala inayopendekezwa na Iran kupitia Mlango Bahari wa Hormuz litaongeza mvutano katika eneo la Mashariki ya Kati.
Araghchi amesema hatua ya kupuuza njia hiyo inaweza kuchochea mzozo mpya, hasa ikizingatiwa kuwa Mlango Bahari wa Hormuz ni njia muhimu kwa usafirishaji wa mafuta duniani.
Kauli yake ameitoa katika wakati ambapo mashambulizi mapya yameripotiwa katika eneo la Ghuba, yakionyesha udhaifu wa makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyosimamiwa na Pakistan mnamo mwezi Februari. Makubaliano hayo yalilenga kumaliza kile Iran inachokiita vita vilivyoanzishwa na Marekani na Israel, ambavyo vimesababisha kuyumba kwa masoko ya nishati na kutatiza usafirishaji wa meli.
Ingawa usitishaji mapigano ulianza kutekelezwa mwezi Aprili, mashambulizi ya mara kwa mara yameendelea kushuhudiwa, hasa dhidi ya meli zinazopita katika Mlango Bahari wa Hormuz. Mivutano hiyo imekuwa ikichochewa na hatua za kijeshi za pande zote - Tehran na Washingto, na imeongeza wasiwasi wa kimataifa kuhusu usalama wa njia za baharini.
Hali ilizidi kuwa tete wiki hii baada ya Oman kutangaza njia mbadala ya usafiri wa meli katika Mlango Bahari wa Hormuz, njia inayofuata ukanda wa pwani wa Oman. Serikali ya Muscat ilisema kuwa hatua hiyo ilichukuliwa kwa ushirikiano na Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Majini (IMO), ili kuhakikisha usalama wa meli zinazopita katika eneo hilo.
Hata hivyo, Tehran ilionyesha kukasirishwa na tangazo hilo, ikidai kuwa hatua ya Oman inaweza kudhoofisha msimamo wa Iran katika kulinda mamlaka yake ya baharini na inaweza pia kuathiri usalama wa njia za kimkakati za usafirishaji.