Wakati wananchi wa Manyara wakilalamika kulipwa fidia ndogo waliyolipwa kupisha ujenzi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limesema malipo hayo yamezingatia taratibu zote za ulipaji fidia za kitaifa na kimataifa.
Akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi, Mei 30, 2024 Mkurugenzi wa TPDC, Musa Makame amesema hakuna taratibu zilizokiukwa na kuwataka wasioridhika na fidia hiyo kufuata taratibu za kufikisha malalamiko yao.
Taratibu hizo Makame amesema zinaanzia ngazi ya kijiji, wilaya na mkoa na kama wataona hawajaridhika ofisi zao zipo wazi huku akibainisha mpaka sasa hajafikiwa na malalamiko yoyote mezani kwake.