Waziri wa Mambo ya Nje wa Ukraine, Adrii Sybiha, ameituhumu Hungary kwa kuwateka nyara wafanyakazi wa benki wa Ukraine waliokuwa wakisafirisha dola milioni 40 na kilo tisa za dhahabu mapema leo.
Sybiha ameandika kwenye mtandao wa X kwamba raia saba wa Ukraine wanaofanya kazi na benki ya serikali, Oschadbank, walitekwa mjini Budapest wakati wakiwa na magari ya benki hiyo yanayosafirisha fedha kutokea Austria.
Benki hiyo imethibitisha kukamatwa kwa wafanyakazi hao ambapo Sybiha ameituhumu Hungary kwa kile alichokiita utekaji nyara na wizi wa fedha hivyo hakukuwa na majibu ya mara moja kutoka serikali ya Hungary kufuatia tuhuma hizo za Ukraine.
Hata hivyo Hungary ni mojawapo ya mataifa machache ya Ulaya yanayoendelea kuwa na uhusiano mzuri na Urusi tangu uvamizi wake dhidi ya Ukraine na imekuwa daima ikipinga msaada wa kijeshi kwa Kiev.
#10YrsJembefm #Familiamoja #AhsantekwaTime