Nchini Cameroon, vifo vitatu katika siku chache tu huko Bamenda na vitongoji vyake vinatumika kama ukumbusho dhahiri kwamba ukosefu wa usalama bado umeenea katika mji mkuu wa jimbo la Kaskazini Magharibi mwa nchi linalozungumza Kiingereza. Kiwango hiki cha juu cha vurugu kinachoendelea kinahusishwa na uwepo mkubwa wa silaha za moto zinazosambazwa kufuatia miaka kumi ya mgogoro usiotatuliwa katika maeneo yanayozungumza Kiingereza.
Nchini Cameroon, mwathiriwa wa kwanza anaripotiwa kufariki kutokana na majeraha baada ya kupigwa risasi wakati wa shambulio la utekaji nyara siku ya Ijumaa ya wiki iliyopita kwenye gari lililokuwa limebeba watu kadhaa wakirudi kutoka mazishi. Mwathiriwa mwingine alipatikana amepigwa hadi kufa siku ya Jumatatu asubuhi. Mtu wa tatu anaripotiwa kupigwa risasi akiwa njiani kurudi nyumbani kutoka kazini.
Kwa Fon Nsoh, kiongozi maarufu katika mshirika ya kiraia na mratibu wa shirika lisilo la kiserikali la Cominsud, ambalo linafanya mkutano huko Bamenda leo Alhamisi kujadili hali hiyo, vurugu hizi zinahusishwa na upatikanaji mkubwa wa silaha za moto.
"Hali huko Bamenda bado haitabiriki. Haiwezekani kujua ni wapi na lini unaweza kuanguka mikononi mwa watu wasiofaa, kushambuliwa, au hata kuuawa. Tunafahamu visa ambapo watu wametekwa nyara mchana kweupe mapema saa 11 jioni. Ukosefu huu wa usalama ni matokeo ya kuongezeka kwa silaha za moto." Watu binafsi huzitumia kupora pesa, wengine huajiri wauaji ili kutekeleza ulipizaji kisasi. Mgogoro huu na vurugu umeendelea kwa miaka kumi. Lazima tutafute njia za kuumaliza na kujenga upya jamii. “Tukiacha mambo yaendelee kama yalivyo, tunaweza kupitia miaka mingine kumi ya mgogoro bila washindi au kushindwa, lakini familia nyingi zitaendelea kupoteza wapendwa wao,” amesema.
Kiongozi wa Kanisa la Anglikana, Sarah Mullaly, Askofu Mkuu wa Canterbury, anatarajiwa mjini Yaoundé, siku ya Ijumaa kwa ziara ya siku tano, karibu miezi minne baada ya ziara ya Kiongozi wa Kanisa Katolika duniani, Papa Leo XIV, huko Bamenda kujadili amani. Hizi ni ziara muhimu, kulingana na Fon Nsoh, lakini matokeo yao halisi bado yanasubiriwa, anasema.